HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA , MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE,

KWENYE SHEREHE ZA KUADHIMISHA MIAKA 45 YA UHURU WA TANZANIA BARA, UWANJA WA TAIFA,

DAR ES SALAAM, TAREHE 09 DESEMBA, 2006

Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni,

Rais wa Jamhuri ya Uganda;

Mheshimiwa Levy Mwanawasa, Rais wa Jamhuri ya Zambia;

Mheshimiwa Mwai Kibaki, Rais wa Jamhuri ya ;

Mheshimiwa Armando Guebuza, Rais wa Jamhuri ya Msumbiji;

Mheshimiwa Dkt. Bingu wa Mutharika,

Rais wa Jamhuri ya Malawi;

Mheshimiwa Ahmed Abdullah Mohamed Sambi,

Rais wa Comoro;

Mheshimiwa Pakalitha Mosisili, Waziri Mkuu wa Lesotho;

Mheshimiwa Marine Barampama, Makamu wa Pili wa

Rais wa Burundi;

Mheshimiwa Dkt. ,

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

Mheshimiwa Aman ,

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ; Mheshimiwa Edward Ngoyai Lowassa,

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

Mheshimiwa ,

Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar;

Mheshimiwa Samuel Sitta,

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

Mheshimiwa Barnabas Samatta, Jaji Mkuu wa Tanzania;

Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu wa

Awamu ya Pili;

Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu;

Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu;

Mheshimiwa Mama Maria Nyerere;

Mheshimiwa Mama Fatma Karume;

Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge;

Waheshimiwa Mabalozi;

Waheshimiwa Viongozi wa ngazi mbalimbali wa

Vyama vya Siasa;

Wageni Waalikwa;

Mabibi na Mabwana.

Ndugu Wananchi; Leo ni siku ya aina yake katika historia ya nchi yetu. Ni siku ambayo miaka 45 iliyopita tulikata minyororo ya ukoloni. Tarehe kama ya leo, mwaka 1961, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alituongoza wananchi wa , wakati ule, katika kuupokea uhuru wetu na wa nchi yetu. Ni siku ambayo aibu ya takriban miaka 77 ya kutawaliwa na wageni ilikoma. Yaani tulitawaliwa na Waingereza kwa miaka 43 (1918 – 1961) na kabla yao miaka 34 (1884 – 1918) ya ukoloni wa Ujerumani.

Ndiyo siku lilipozaliwa taifa huru la watu wa Tanganyika, ambayo sasa ni Tanzania Bara kufuatia kuungana na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar Aprili 26, 1964 na kuzaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ndugu zangu;

Wananchi Wenzangu;

Leo ni siku ambayo kila Mtanzania popote alipo, ndani na nje ya nchi yetu, anayo kila sababu ya kufurahi na kusherehekea. Natambua kwamba zaidi ya theluthi mbili ya Watanzania tuliopo sasa hawakuwepo wakati ule. Wakati ule nchi yetu ilikuwa na watu milioni 9 tu ukilinganisha na sasa ambapo tuko watu milioni 36. Hata hivyo, wote tunawajibika kusherehekea siku ile kwa sababu ndiyo siku ya ukombozi wetu sote, kwani kama uhuru usingepatikana siku ile huenda hata leo tungekuwa kwenye harakati za kupigania uhuru.

Ndugu Wananchi;

Katika kusherehekea siku hii kubwa hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwanza kwa kutuweka hai na kutufikisha salama siku ya leo. Pili, kwa kuiangazia nuru njema nchi yetu, kuilinda na kuiwezesha kuwa na amani, umoja, upendo na mshikamano thabiti kwa kipindi chote cha miaka 45 ya uhuru wetu. Wakati tunaadhimisha miaka 45 ya Uhuru wa Tanganyika, ni siku pia ya kusherehekea na kuwakumbuka wazee wetu waliojitolea muhanga kupambana na mkoloni mpaka akasalimu amri na kuondoka. Wengi wa wazee wetu hao akiwemo jemadari mkuu wa mapambano hayo Baba wa Taifa, hayati Mwalimu wameshatangulia mbele ya haki. Lakini, wapo pia wengi kiasi ambao bado wako hai na baadhi yao tunao hapa leo.

Naomba nitambue kuwepo kwa Chifu Patrick Kunambi, Mzee Ally Sykes, Mzee C. Milinga na Mzee Suleiman Kitwara ambao pamoja na wenzao 12 chini ya uongozi wa Mwalimu Julius Nyerere walianzisha Chama cha Ukombozi cha TANU tarehe 07 Julai, 1954. Uamuzi wao wa busara na moyo wao wa ushujaa na ujasiri wa kuongoza harakati za kupigania uhuru na ukombozi wa Tanganyika ndiyo uliozaa Tanganyika huru. Kwa kweli leo ni siku yao ya kuwakumbuka na kuwashukuru kwa wema mkubwa walioifanyia nchi yetu na sisi watu wake.

Wakati tukiwakumbuka na kuwashukuru waasisi wa Chama cha Tanu tunafanya hivyo pia kwa wazee wote wengi waliojiunga nao katika harakati hizo. Wengi hawako nasi duniani, tunawatakia mapumziko mema. Lakini wapo wengi tunao miongoni mwetu na bahati nzuri baadhi yao tunao hapa leo wakiongozwa na Simba wa Vita mzee wetu Rashid Mfaume Kawawa. Nyote tunawashukuru sana.

Katika siku ya leo, tunapowakumbuka wazee wetu waliojitolea muhanga kwa ajili ya uhuru na ukombozi wa nchi yetu, pia tunawakumbuka wale wote walioanzisha harakati za kuukataa ukoloni hata kabla ya kuzaliwa kwa Chama cha TANU. Natambua juhudi za mashujaa wa vita vya Maji Maji kuanzia Kilwa hadi Songea, mashujaa wa Kihehe na Kichaga na wengineo wengi. Katika kukataa kutawaliwa baadhi yao walipoteza maisha. Wao ndio waliopanda mbegu ya awali iliyokuja kuchipua katika TANU na kuzaa tunda tunalolisherehekea leo.

Ndugu Wananchi; Wakati tukisherehekea miaka 45 ya Uhuru wa nchi yetu, ni siku pia ya kutafakari tulikotoka, tulipo sasa na kuangalia mbele tuendako. Ni dhahiri kabisa kwamba ukilinganisha tulipo sasa na kule tulikotoka miaka 45 iliyopita tumepiga hatua kubwa sana. Katika nyanja zote za maisha ya mwananchi wa Tanzania Bara tumepata maendeleo makubwa ukilinganisha na pale alipotuacha mkoloni. Tumefaulu.

Umoja wa Kitaifa

Ndugu Wananchi wenzangu;

Kwa sababu ya sera yake ya “wagawe uwatawale” (divide and rule) mkoloni alituacha wananchi wa Tanganyika wakati ule tukiwa tumegawanyika kwa makundi makundi.

Mkoloni alituacha tukiwa tumegawanyika kwa makabila yetu, kwa dini zetu na kwa rangi zetu. Kila kabila na chifu wake, mtemi wake au mtawala wake wa jadi lilikuwa ni taifa pekee. Watu walitambuana, kushirikiana na kusaidiana kwa dini zao au kwa rangi zao na makabila yao. Hata kwa watu wa kabila moja walibaguana kwa maeneo watokako.

Kadhalika watu waliishi na huduma zilitolewa kwa misingi ya rangi zao. Miji ikawa na mitaa ya Uzunguni, Uhindini na Uswahilini. Hivyo hata huduma za elimu, afya, maduka, burudani, uchumi na hata makaburi yaligawanywa hivyo hivyo. Lakini baya zaidi hata thamani ya utu wao ilipewa daraja kwa misingi ya rangi ya ngozi zao ambapo mtu Mweusi alikuwa na daraja la chini, Muasia la kati na Mzungu ndiyo mbora wa wote. Mswahili alikuwa haruhusiwi kupanda ndege bila kudhaminiwa na Mzungu, au Muhindi au Mwarabu kwani kwa ushamba wake eti anaweza kutapika akachafua ndege au hata kufanya vurugu angani kwa hofu zake. Hata bia Mwafrika alikuwa haruhusiwi kunywa maana stahili yake ni dengerua na inapouzwa panaitwa Mwafrika Bar au Pombe shop. Uchumi nao ulikuwa mikononi mwa Wazungu na Waasia. Biashara ndogo ndogo zilikuwa mikononi mwa Waarabu na Mwafrika alikuwa mtumishi wa wote hao. Ni kibarua anayelipwa ujira mdogo sana na muda mwingi kuambulia matusi na hata makofi. Hiyo ndugu zangu ndiyo sura ya maisha ya wananchi wa Tanganyika wakati tunapata uhuru. Nchi yetu haikuwa taifa moja la watu wamoja, wanaoishi pamoja na kushirikiana. Lilikuwa ni taifa la mkusanyiko wa watu ambao kila mmoja na lwake. Watu wanadharauliwa na kunyanyaswa chini ya utawala wa mkoloni Mwingereza. Uhuru ulimkomboa Mwafrika wa Tanganyika dhidi ya manyanyaso na ulimrejeshea heshima yake na utu wake ulioporwa na wakoloni. Katika mazingira hayo basi kazi ya kwanza iliyofanywa na Serikali ya Tanganyika huru ilikuwa kumjenga mwananchi ajiamini kuwa yuko huru. Pili, kujenga taifa la watu wamoja, wanaoishi kwa upendo na ushirikiano kama taifa. Hii ilikuwa ndiyo changamoto kubwa ya kwanza ya Serikali ya Tanganyika huru.

Chini ya uongozi mahiri na shupavu wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kazi ya kujenga taifa moja ilifanyika kwa ufanisi wa hali ya juu. Ukabila, udini, ubaguzi wa rangi na ubaguzi kwa mujibu wa maeneo vilizikwa. Watu walikuwa hawatangulizi dini, kabila, rangi au eneo atokalo kama sharti la kuishi au kushirikiana na mwenzake.

Ndugu Wananchi;

Lakini, katika kujenga umoja, Mwalimu Nyerere aliisogeza Tanganyika hatua moja zaidi. Kwa kushirikiana

na mwana mapinduzi shupavu, Mzee Abeid Amani Karume aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar waliunganisha nchi zao mbili huru na kuzaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Leo tunaposherehekea miaka 45 ya Uhuru wa Tanganyika tunasherekea nchi ambayo imefanikiwa kujenga umoja miongoni mwa watu wake na miongoni mwao na ndugu zao wa nchi huru ya Zanzibar. Bahati nzuri, bado misingi ya umoja wa wananchi na taifa letu ni imara pamoja na misukosuko ya hapa na pale ambayo imekuwa inatokea katika vipindi na nyakati mbalimbali. Muungano ni imara na inshallah Mwenyezi Mungu atatujalia utapanda daraja na kuwa Shirikisho la Afrika Mashariki. Bado udini, ukabila, ubaguzi wa rangi au wa eneo ni mambo yanayopingwa na kukataliwa na Watanzania walio wengi. Bado ni misingi inayoongoza maadili ya utaifa na mahusiano baina ya watu wa nchi yetu.

Ndugu Wananchi;

Wahenga wamesema usione vinaelea vimeundwa. Waundaji wa umoja na mshikamano wa watu wa nchi yetu si wengine bali ni sisi wananchi wenyewe, chini ya uongozi bora wa viongozi wa nchi yetu na serikali zetu mbili tangu enzi za Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume. Misingi mizuri na imara ya umoja waliyoiweka na kuzingatiwa na viongozi wa awamu zote zilizofuatia kwa upande wa Muungano na Zanzibar, ndiyo iliyoiwezesha nchi yetu kuwa na amani, usalama na utulivu tuliokuwa nao sasa. Ndiyo inayowafanya Watanzania kuwa na umoja, mshikamano na ushirikiano pamoja na tofauti zao za rangi, kabila, dini, maeneo watokako au hata kwa sasa tofauti ya ufuasi wa vyama vya siasa.

Ni misingi mizuri na maadili mema ambayo katika kusherehekea miaka 45 ya uhuru wetu hatuna budi kuazimia kuidumisha. Tena tuidumishe kwa hali na mali na kwa wakati wote, iwe jua au mvua.

Maendeleo ya Kiuchumi na Kijamii

Ndugu Wananchi;

Kwa upande wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii nayo tumepata mafanikio makubwa. Hali ya maisha ya Watanzania ilivyo leo sivyo ilivyokuwa wakati tunapata Uhuru. Bado nchi yetu ni maskini na watu wetu wengi ni maskini, lakini hali yao ni bora zaidi sasa kuliko ilivyokuwa mwaka 1961. Watu wengi zaidi sasa wana kipato kikubwa, wanaishi katika nyumba bora, wanavaa vizuri, wanakula vizuri, wanapata elimu, wanapata huduma za afya, maji na barabara kuliko ilivyokuwa zamani. Serikali inao uwezo mkubwa zaidi wa kuwahudumia wananchi wake kuliko ilivyokuwa ingawaje watu wameongezeka mara 4 na mahitaji yameongezeka pia.

Hata hivyo, ndugu zangu, kwa kiwango cha maendeleo tulichonacho bado tunayo kazi kubwa ya kufanya. Hivyo basi katika kusherehekea miaka 45 ya uhuru wa nchi yetu tuazimie kuendeleza mapambano dhidi ya umaskini na kuwa nyuma kimaendeleo, kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya.

Elimu

Ndugu Wananchi;

Wakati tunapata uhuru hali ya upatikanaji wa elimu nchini ilikuwa ni duni sana. Sehemu ndogo sana ya watu wetu waliweza kupata elimu. Hivyo, watu wengi walikuwa wanakabiliwa na tatizo la ujinga. Ndiyo maana Mwalimu Nyerere aliutangaza ujinga kuwa moja ya maadui watatu wa nchi yetu pamoja na umaskini na maradhi. Hali ilikuwa hivyo kwa sababu ya ufinyu wa fursa za kupata elimu hasa kwa Waafrika. Kwa sababu ya ubaguzi Serikali ya ukoloni

haikujali na hivyo haikujihusisha vya kutosha na elimu kwa wananchi. Kazi hiyo iliachiwa mamlaka za wenyeji na mashirika ya dini na hasa makanisa kuifanya pale ambapo yalipobahatika kuwepo.

Hata pale Serikali ilipojihusisha ilijali zaidi elimu ya kupata makarani tu na siyo kupata watu wenye taaluma muhimu kwa maendeleo kama vile udaktari, uhandisi na kadhalika. Kwa jumla, wakoloni walikuwa na sera ya makusudi ya kutokuwasomesha Waswahili ili wawatawale vizuri.

Ndugu Wananchi;

Kwa ajili hiyo, wakoloni walipoondoka kulikuwa na shule za msingi zipatazo 3000 zenye wanafunzi 486,000 tu. Kutokana na juhudi zetu wenyewe baada ya uhuru, hivi sasa tuna shule za msingi 11,560 zenye wanafunzi 7,957,884. Aidha, tulipopata uhuru nchi yetu ilikuwa na shule za sekondari 54 na Seminari 9 tu zote zikiwa na jumla ya wanafunzi 13,897. Hivi sasa tunazo shule za Sekondari za Serikali 1,715 na zisizo za Serikali 640. Zote kwa pamoja zina jumla ya wanafunzi 675,672. Nia yetu ni kuendelea kuongeza shule za sekondari ili kila kata nchini iwe na angalau sekondari moja. Hii itatuwezesha kuwa na sekondari mpya zaidi ya 2556 za serikali katika miaka mitano ijayo.

Ndugu zangu, Wananchi Wenzangu;

Wakoloni hawakutuachia Chuo Kikuu hata kimoja. Hivyo walipoondoka nchi yetu ilikuwa na uhaba mkubwa wa wazalendo wenye elimu ya Chuo Kikuu. Baada ya uhuru ndipo jitihada kubwa ya kuwasomesha wananchi kupata elimu hiyo ilipoanza kwa dhati. Chuo Kikuu Kishiriki cha kwanza nchini kilianzishwa mwaka 1961 kwa uamuzi wa TANU kujitolea jengo lake kwa ajili hiyo. Kilianza na wanafunzi 14 wa Kitivo cha Sheria.

Leo hii nchini tunavyo Vyuo Vikuu kamili na Vishiriki vya Serikali na binafsi vipatavyo 22 vyenye wanachuo 40,881 wakiwemo wanawake 13,145 na wanaume 27,736. Nia yetu ni kuendelea kupanua elimu ya Chuo Kikuu, Elimu ya Juu na mafunzo ya taaluma kwa jumla hapa nchini. Lengo letu ni kutaka watu wengi zaidi wapate nafasi ya kujiendeleza na hivyo kuongeza kasi ya kuleta maendeleo nchini. Tunaamini, kufanya hivyo kutasaidia sana katika kuboresha maisha ya wananchi na kuendeleza taifa letu.

Afya Ndugu Wananchi;

Kwa upande wa huduma ya afya hali nayo ilikuwa kama elimu. Huduma ilikuwa duni na haitoshelezi mahitaji na ya kibaguzi ambapo afya ya wananchi haikupewa umuhimu stahiki. Watu wengi waliishi kwa kutegemea miti shamba na waganga wa asili. Mafanikio mengi tumeyapata kwenye sekta ya afya kwa kazi kubwa iliyofanywa tangu baada ya uhuru mpaka sasa.

Tumefanikiwa kuongeza idadi ya hospitali kutoka 98 zilizokuwapo wakati tunapata uhuru hadi kufikia hospitali 219 hivi sasa. Zahanati nazo zimeongezeka kutoka 236 mwaka 1961 hadi 4,679 hivi leo. Tumeongeza pia idadi ya vituo vya afya vijijini kutoka vituo 22 tulivyorithi kutoka kwa wakoloni hadi vituo 481 vya sasa.

Watu wengi zaidi sasa wanapata huduma ya afya kuliko ilivyokuwa wakati wa ukoloni. Afya za Watanzania wengi zimeimarika zaidi sasa kuliko ilivyokuwa. Watu sasa wanaishi miaka mingi zaidi na ndiyo maana idadi ya watu ni mara nne ya wale waliokuwepo wakati nchi yetu inapata uhuru. Bado tunayo kazi kubwa ya kuboresha huduma ya afya nchini kwa kujenga zahanati na vituo vya afya na hospitali zaidi. Kuboresha huduma ya watoto na mama wajawazito na kupambana na maradhi yanayoua watu wengi kama vile malaria, ukimwi, kifua kikuu na mengineyo. Kazi hiyo tunaendelea nayo vizuri.

Ndugu Wananchi;

Hatuwezi kuzungumzia mafanikio yetu kwa kipindi chote cha miaka 45 ya uhuru wetu bila kugusia suala la miundombinu. Tangu tupate uhuru Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kupanua huduma za usafiri wa barabara, reli, anga na usafiri wa majini.

Tumepata mafanikio makubwa na ya kutia moyo. Maeneo mengi vijijini sasa yanafikika kwa barabara. Kwa mfano, tumepanua mtandao wa barabara nchini hadi kufikia kilomita 85,000. Changamoto yetu ni kuzifanya barabara hizo zipitike wakati wote. Kwa shabaha hiyo tumeongeza barabara za lami kutoka kilometa 1300 zilizokuwapo mwaka 1961 hadi kufikia kilomita 4,837 hivi sasa. Mipango ipo ya kuongeza idadi ya barabara za lami na utekelezaji unaendelea maeneo mengi nchini hivi sasa.

Kama mjuavyo, ndugu wananchi, uchumi ni mawasiliano. Bila miundombinu bora uchumi wetu hauwezi kukua haraka. Pia panapokuwepo na barabara watu hutumia magari badala ya kutembea kwa miguu, hivyo kufanya maisha kuwa rahisi na bora zaidi. Serikali itaendelea na kazi ya kukamilisha programu ya uwekezaji katika sekta ya miundombinu ili kurahisisha mawasiliano na hivyo kuchochea kukua kwa shughuli za kiuchumi na kibiashara hapa nchini. Tutaendelea kuimarisha reli zetu za TRC na TAZARA na tutaongeza viwanja vya ndege pamoja na kuviimarisha na kuboresha vilivyopo. Tutaimarisha na kupanua usafiri wa majini vile vile. Kadhalika, tutaendelea kupanua huduma ya simu nchini. Hili ni eneo ambalo tumefanikiwa vizuri sana kwani sehemu nyingi za nchi mawasiliano ya simu yanapatikana. Mkoloni ameacha huduma hii ikiwa duni sana tena ya kizamani.

Ndugu Wananchi;

Eneo lingine muhimu ambalo tumefanikiwa kupata mafanikio makubwa ni la ulinzi na usalama. Nchi yetu imeendelea kuwa huru, salama na yenye utulivu kwa sababu ya uimara na kazi nzuri inayofanywa na majeshi yetu ya ulinzi na usalama. Lakini siri kubwa ya mafanikio hayo ni kule kuibadili falsafa ya majeshi yetu kutoka kuwa ya kukandamiza raia na kuwa majeshi ya umma ya kutetea, kulinda na kudumisha haki na maslahi ya raia na ya nchi yao.

Leo tunaposherehekea uhuru wetu, sote tumeshuhudia ni jinsi gani majeshi yetu yalivyo tayari kulinda mipaka na usalama wa nchi yetu na raia wake. Kwa misingi hiyo majeshi yetu yameweza kulinda mipaka ya nchi yetu isichezewe kama yalivyofanya mwaka 1978-80 tulipovamiwa na nduli Iddi Amin wa Uganda. Kadhalika majeshi yetu yamekuwa chombo imara cha kulinda usalama wa maisha na mali za raia. Pamoja na hayo, majeshi yetu yametoa mchango wa pekee katika harakati za ukombozi Kusini mwa Afrika. Tutaendelea kuyajenga na kuyaimarisha majeshi yetu kwa watu, mafunzo, zana na vifaa ili kudumisha uimara wake na umahiri wake. Miongoni mwa mambo ambayo tutayaendeleza kwa uwezo wetu wote ni mafunzo ya ulinzi wa mgambo. Mafunzo haya yanawapa wananchi wenyewe maarifa na uwezo wa kulinda usalama wa nchi yao pamoja na usalama wao wenyewe na mali zao. Manufaa ya mafunzo ya mgambo tuliyaona wakati wa Vita ya Kagera ambapo walinzi wa mgambo walitoa mchango mkubwa sana.

Ndugu Wananchi;

Naweza kuendelea kuyataja mafanikio zaidi tuliyoyapata tangu tuwe taifa huru. Lakini nachelea kufanya hivyo kwa kutopenda kuwachosha. Naelewa ninyi mnayafahamu vizuri mafanikio yote tuliyopata hadi sasa. Pia mnaelewa vizuri matatizo yaliyotukabili huko nyuma na yale yanayoendelea kutukabili hivi sasa katika jitihada zetu

za kujenga nchi yetu. Hivyo sina sababu ya kuchukua muda wenu kuyaelezea. Jambo la msingi kwetu sote ni kuhakikisha kuwa tunayalinda vizuri mafanikio tuliyokwishayapata na kuongeza juhudi za kupata mafanikio mengi zaidi ili kuharakisha maendeleo yetu. Tutafanya kila tuwezalo kukabiliana na matatizo yaliyopo mpaka ushindi kamili.

Ndugu Wananchi;

Katika kulinda mafanikio tuliyokwishayapata na kudumisha uhuru wetu, Serikali itaendelea kutekeleza mipango mbalimbali yenye lengo la kuimarisha uchumi wetu na kuboresha maisha ya kila mmoja wetu. Baadhi ya mipango hiyo tumeanza kuitekeleza ikiwemo Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Kilimo unaolenga katika kuleta mapinduzi makubwa ya kilimo hapa nchini.

Aidha, Serikali itaendelea kujenga mazingira mazuri ya kiuchumi na kibiashara ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza zaidi nchini mwetu. Pia tutahakikisha kuwa vikwazo vinavyokwamisha uanzishaji na uendeshaji biashara hapa nchini vinaondolewa mapema ili kuimarisha sekta ya biashara na uwekezaji ambayo ni muhimu sana katika kuleta ajira nchini. Vile vile tutaendelea na jitihada tulizokwishazianza, kupitia mpango wa MKURABITA, MKUKUTA na mingineyo, za kuwawezesha wananchi kiuchumi kwa kuwajengea uwezo wa kushiriki kwa ukamilifu katika ujenzi wa uchumi wa nchi yao. Katika kufanya hivyo na wao wanainua kipato chao na kuboresha hali yao ya maisha.

Uhuru na Kazi

Ndugu zangu, Wananchi Wenzangu;

Ombi langu kwenu leo ni moja. Nawaombeni kila mmoja wetu afanye kazi kwa bidii na maarifa ili kwa pamoja tusukume mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu.

Yule aliyeko kiwandani afanye kazi kwa bidii, aliyeko shambani naye afanye kazi kwa bidii na aliyeko ofisini pia afanye kazi kwa bidii. Kauli ile ya Uhuru na Kazi bado ina maana sasa kama ilivyokuwa wakati ule. Sisi sote tufanye kazi kwa bidii kwani Uhuru ni Kazi.

Naamini kabisa tukizingatia na tukifanya hivyo tutafanikiwa haraka katika kujenga uchumi imara na wa kisasa. Hiyo ndiyo nguzo kuu ya kulinda na kuimarisha uhuru wa taifa letu. Suala la kufanya kazi kwa bidii, ndugu zangu, naombeni sana tulizingatie kwa makini. Hakuna njia ya mkato au badala yake ya kupatia maisha bora tunayoyaimba. Nchi yetu itajengwa kwa kila mmoja wetu kufanya kazi kwa bidii na maarifa.

Ndugu Wananchi; Naomba nimalize kwa shukrani. Kwanza, nawashukuru wageni wetu wote kwa kukubali mwaliko

wetu wa kuja kujumuika nasi hapa leo. Kwa niaba yenu napenda kutoa shukrani za kipekee kwa Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka nchi jirani walioko hapa kwa heshima kubwa waliyotupa. Kuwepo kwao hapa ni ishara ya urafiki na udugu uliopo baina ya nchi zao na nchi yetu. Kwao wote nasema asanteni sana.

Aidha, napenda kwa niaba yenu niwashukuru wale wote walioandaa sherehe hizi. Zimefana sana kwa sababu ya juhudi zao. Namshukuru Waziri Mkuu, Mheshimiwa kwa uongozi wake mzuri. Wanajeshi wetu wa vyombo vya ulinzi na usalama kwa gwaride zuri kama ilivyo kawaida yao. Walimu na wanafunzi kwa halaiki murua yenye mafunzo na kuburudisha. Wasanii wote kwa tumbuizo zao.

Mwisho, napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru tena nyote wananchi wenzangu. Kwanza, nawashukuru kwa kufanikisha maadhimisho haya leo kwa kujitokeza kwa wingi kama mlivyofanya. Pili, kwa kudumisha na kuimarisha uhuru wa nchi yetu. Nyinyi ndiyo mwanzo na mwisho wa uhuru wetu. Bila nyinyi hakuna uhuru.

Ni juhudi zenu ndizo zimeifikisha nchi yetu hapa tulipo leo. Na juhudi zenu ndizo zitakazodumisha uhuru wetu na ndizo zitakazoitoa nchi yetu hapa tulipo sasa na kuisogeza mbele kimaendeleo. Tukumbuke kuwa daima mjenga nchi ni mwananchi. Hakuna mtu mwingine atakayekuja kutujengea nchi yetu ila sisi wenyewe.

Hivyo basi , ndugu zangu, tunaposherehekea siku hii adhimu ya uhuru wetu, hatuna budi tuamue kwa dhati kuwa tunataka kuijenga nchi yetu ili iendelee kuwa mahali pazuri pa kuishi kwa ajili yetu sisi wenyewe, watoto wetu na watoto wa watoto wetu. Mimi naamini kabisa kuwa hili linawezekana ikiwa sote tutadhamiria hivyo. Tukumbuke msemo maarufu wa muasisi wa taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere usemao: Inawezekana, timiza wajibu wako. Basi tukifanya hivyo kuanzia leo, kesho na keshokutwa, miaka michache ijayo tutakuwa taifa lenye maendeleo makubwa zaidi kuliko tulivyo sasa.

Tanzania yenye neema inawezekana!

Mungu Ibariki Afrika!

Mungu Ibariki Tanzania!

Asanteni kwa kunisikiliza.